HABARI ZA SIASA

Hofu ya serikali yawafanya wahamishe wanafunzi

Mwenyekiti wa KEPSA, Bw John Mwai

Picha/MAKTABA Mwenyekiti wa Chama cha Shule za Kibinafsi, Bw John Mwai (kushoto) akiwa na Mwekahazina wa chama hicho, Bw Kabiru Ndiritu, kwenye kikao na wanahabari Januari 18, 2012. 

Na WAANDISHI WETU  ( email Mwandishi)

Imepakiwa - Saturday, February 18  2012  at 18:7

Kwa Mukhtasari

Wazazi wanahamisha wanafunzi kutokana na mfumo wa uteuzi wa wanafunzi wanaojiunga na kidato cha kwanza, ambao kwa miaka mitatu sasa umeonekana kuwapendelea wanafunzi wa shule za umma.

WAZAZI wengi wameanza kuwaondoa watoto wao kutoka shule za msingi za kibinafsi na kuwapeleka kwa zile za umma.

Chama cha shule za kibinafsi na kile cha wazazi, vimekiri kuwa kuna uhamishaji wa kiwango cha juu wa wanafunzi, hasa wa madarasa ya saba na nane.

Shule nyingi za msingi za umma sasa zina msongamano mkubwa wa wanafunzi.

Hali hii inatokana na mfumo wa uteuzi wa wanafunzi wanaojiunga na kidato cha kwanza, ambao kwa miaka mitatu sasa umeonekana kuwapendelea wanafunzi wa shule za umma.

Baadhi ya wazazi wameshutumiwa kwa kuungana na walimu wakuu wa shule za msingi za umma, ili watoto wao wasajiliwe kufanya mitihani yao ya KCPE huko, licha ya kuendelea kusoma katika shule za msingi za kibinafsi hadi mtihani wa KCPE uanze.

Usajili wa wanafunzi si siri

Katibu Mkuu wa Chama cha Wazazi (KNAP), Bw Musau Ndunda, alisema usajili wa wanafunzi kutoka shule za kibinafsi katika shule za umma sio siri.

“Sera ya serikali kuwapa wanafunzi wa shule za umma kipaumbele wakati wa kujiunga na kidato cha kwanza imewasababisha wazazi wengi kuungana na walimu wakuu ili watoto wao wasajiliwe kufanya mitihani yao, huku wakiendelea kusoma katika shule za kibinafsi,” alisema.

Bw Ndunda aliambia Taifa Jumapili kuwa, licha ya hatua hii kukiuka sheria, wazazi hawapaswi kulaumiwa kwani kila mmoja ana haki ya kumtafutia mwanawe masomo mema.

Mwenyekiti wa chama cha wamiliki wa shule za kibinafsi KEPSA, Bw John Mwai, alisema mfumo huu mpya pia umesababisha wazazi wengi kuwahamisha watoto wao katika shule za umma za malazi.

Karo imezidi

“Nyingi ya shule hizi ni za hali ya juu na hata karo imezidi inayolipwa katika shule nyingi za kibinafsi. Tofauti na  shule nyingi za kibinafsi, shule hizi kama Nairobi Primary, Muthaiga Primary na Nyeri Complex zina vifaa bora na hivyo zinatoa fursa kwa wanafunzi kukubaliwa katika shule za kitaifa,” asema.

Kulingana na Bw Mwai, huenda hatua hii ikaleta misongamano katika shule hizi na hata kuathiri kiwango cha masomo.

Alhamisi iliyopita, katibu katika Wizara ya Elimu Prof James Ole Kiyiapi aliunda jopo kazi litakaloangalia upya mfumo huo wa uteuzi wa wanafunzi wa kidato cha kwanza.

Ripoti za Timothy Kimei, Pauline Ongaji na Simon Siele

 

Most Popular

Wabunge 175 kutahiriwa Zimbabwe

Wabunge 175 nchini Zimbabwe watapashwa tohara kufikia mwisho wa mwezi ujao katika juhudi za kuhamasisha wanaume

Mwanawe Waziri wa Fedha ajitia kitanzi

MWANAWE Waziri wa Fedha Njeru Githae anadaiwa kujiua nyumbani kwao Runda, Nairobi. Polisi wameanzisha uchunguzi

Polisi waendelea kusaka walioshambulia Mombasa

Polisi wameanzisha msako mkali kutafuta washukiwa waliotekeleza shambulio la kigaidi katika mkahawa wa Bella Vista,

Utengano wakumba ukumbusho wa Wanjiru

Ibada mbili tofauti zilifanywa kuadhimisha mwaka mmoja tangu kifo cha bingwa wa marathon katika Olimpiki Samuel